*Mkuu wa Wilaya kuanza ziara ya uhamasishaji kesho
NA ABRAHAM NTAMBARA
Halmashauri ya Wilaya ya Longido leo, Januari 6, 2026, imefanya kikao cha wadau wa Bima ya Afya kwa Wote kwa lengo la kuweka mikakati ya uhamasishaji kuelekea utekelezaji wa huduma hiyo, itakayozinduliwa rasmi hivi karibuni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Hatua hiyo ni utekelezaji wa ahadi ya Rais Dkt. Samia aliyoitoa wakati wa kampeni, ya kuhakikisha kuwa ifikapo siku 100 tangu kuanza kwa awamu ya pili ya uongozi wake kuanzia Novemba 3, 2025 alipoapishwa, kila Mtanzania anakuwa na Bima ya Afya.
Akifungua kikao hicho kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Longido, Katibu Tarafa wa Tarafa ya Longido, Bw. Alex Wambura, amesema kuwa kufanyika kwa kikao hicho kunadhihirisha kuanza rasmi kwa utekelezaji wa ahadi hiyo ya Rais kwa wananchi.
“Na kabla ya siku hizi 100 kuisha, tutahakikisha tunafika katika kata zote za Wilaya ya Longido kufanya uhamasishaji. Ratiba ya Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya, Salum Kalli, inaanza kesho asubuhi kwa kufanya kikao Kimokouwa, ambapo moja ya ajenda kubwa kabisa itakuwa ni Bima ya Afya kwa Wote. Tunaamini kuwa kabla ya kutimia siku 100, tutakuwa tumemaliza kata zote 20 za Wilaya ya Longido,” amesema Bw. Mwita.
Ameongeza kuwa ziara hiyo ya Mkuu wa Wilaya itajumuisha Wakuu wa Idara na Vitengo vinavyohusika, Watendaji wa Kata pamoja na Wakuu wa Vituo vya Afya, ili kuhakikisha wananchi wa Longido wanapata taarifa sahihi na za kutosha kuhusu masuala ya Bima ya Afya kwa Wote.
Kwa upande wake, Afisa Uanachama wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), Bw. Miraji Kisile, amesema kuwa huduma ya Bima ya Afya kwa Wote inatekelezwa chini ya Sheria Na. 13 ya mwaka 2023, Sura ya 365.
Amesema sheria hiyo inalenga kuweka mfumo wa kitaifa unaohakikisha kila mwananchi anakuwa na bima ya afya, ambapo makundi yote ya wananchi yanajumuishwa na hivyo kuondoa utaratibu wa kulipa fedha taslimu (cash) wakati wa kupata huduma za matibabu.
Bw. Miraji ameongeza kuwa lengo ni kuwa na mfumo madhubuti wa uchangiaji katika sekta ya afya, kwani uchangiaji wa mtu mmoja mmoja huleta changamoto. Ameeleza kuwa wananchi wenye uwezo watachangia, huku wale wasiojiweza wakilipiwa kupitia utaratibu maalum uliowekwa na Serikali.
Naye Mganga Mkuu wa Wilaya ya Longido, Dkt. Mathew Majani, amesema kikao hicho kimewakutanisha Watendaji wa Kata zote 20, Waganga Wafawidhi kutoka vituo vyote 38 vya kutolea huduma za afya, wajumbe wa Kamati ya Menejimenti ya Halmashauri (CMT) pamoja na Kamati ya Huduma za Afya ya Wilaya (CHMT).
Amesema lengo la kikao hicho ni kuwahusisha wadau muhimu katika utekelezaji wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote, na ametoa wito kwa washiriki kuanza kutoa elimu na hamasa katika maeneo yao ili wananchi waweze kujiandikisha na kunufaika na huduma hiyo.
Kwa upande wao, washiriki wa kikao hicho wamesema kikao kimewapa uelewa mpana kuhusu Bima ya Afya kwa Wote na faida zake. Mganga Mfawidhi wa Zahanati ya Kitendeni, Dkt. Fabian Mtalo, amesema mpango huo utamwezesha mgonjwa kupata matibabu kuanzia ngazi ya zahanati hadi Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), kupunguza gharama za matibabu na kupata huduma wakati wowote katika vituo vilivyosajiliwa na Serikali.
Aidha, Mjumbe wa Bodi ya Afya ya Wilaya, Paine Lemashon, amemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuanzisha mpango huo, akisema kuwa utawarahisishia wananchi kupata huduma bora, endelevu na za uhakika za afya.
Arusha- Namanga Road, Longido Town
Postal Address: S.L.P 84 Longido Arusha
Telephone: +255 272 970 793/ 94
Mobile: 0756395889
Email: ded@longidodc.go.tz
Copyright ©2016 Longido DC . All rights reserved.