Maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika yamefanyika kwa mafanikio makubwa katika viwanja vya Shule ya Msingi Namanga wilayani Longido, yakihudhuriwa na viongozi wa serikali, wadau wa maendeleo, wazazi na wanafunzi kutoka maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo.
Mgeni rasmi katika maadhimisho hayo Katibu Tawala wa Wilaya ya Longido, Bi. Rahma Kondo, aliwapongeza wadau wote wanaojihusisha na ustawi wa watoto kwa kushiriki kikamilifu katika maandalizi na utekelezaji wa maadhimisho hayo muhimu.“Napenda kutoa shukrani za dhati kwa wadau wote wanaoshughulika na masuala ya watoto kwa moyo wa kujitolea, pamoja na kushiriki kikamilifu katika maadhimisho haya.
Siku ya Mtoto wa Afrika ni kumbukumbu ya kipekee inayotukumbusha sisi wazazi na walezi juu ya wajibu wetu wa kuhakikisha watoto wanalelewa katika mazingira salama na yenye staha,” alisema Bi. Rahma.
Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Longido, Bw. Rajab Mmbunda alieleza kuwa maadhimisho haya ni jukwaa muhimu la kuwakumbusha wananchi kuhusu haki za msingi za watoto, ikiwa ni pamoja na haki ya kupata elimu, afya, ulinzi, na malezi bora.
Kaulimbiu ya maadhimisho ya mwaka huu ilikuwa: “Haki ya Mtoto: Tulipotoka, Tulipo na Tuendako,”ikilenga kutathmini hatua zilizopigwa katika kulinda haki za watoto, changamoto zilizopo na mikakati ya kuimarisha ustawi wa watoto barani Afrika.
Mashirika mbalimbali yasiyo ya kiserikali yalijitokeza kushiriki na kutoa mchango wao mkubwa katika tukio hilo. Miongoni mwa mashirika hayo ni ACE Africa, CORDS Tembo, Compassion International, na MPDI, ambayo yameendelea kuwa sehemu muhimu ya maendeleo ya mtoto katika wilaya ya Longido kupitia miradi mbalimbali ya elimu, afya, lishe na ulinzi wa mtoto.Maadhimisho hayo yalipambwa na nyimbo,maigizo ngonjera kutoka kwa watoto na wadau mbalimbali.
Arusha- Namanga Road, Longido Town
Postal Address: S.L.P 84 Longido Arusha
Telephone: 027-2539603
Mobile: 0756395889
Email: ded@longidodc.go.tz
Copyright ©2016 Longido DC . All rights reserved. Designed by Loth Zacharia & Joseph Peter Mkumbwa Sponsored by GWF TAMISEM