Na Happiness Nselu – Longido
Uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Longido umeonyesha kuthamini mchango wa viongozi wa Baraza la Madiwani waliomaliza muda wao, kupitia kikao kifupi cha kuagana kilichofanyika leo tarehe 20 juni 2025 katika ukumbi mdogo wa halmashauri hiyo.
Katika kikao hicho, Mwenyekiti wa Halmashauri Mhe. Simoni Oitesoi na Makamu Mwenyekiti Mhe. Peter Lekanet waliowakilisha Madiwani wengine, walipongezwa kwa uongozi wao wa hekima, busara na uwajibikaji uliosaidia kuleta mageuzi makubwa katika Halmashauri hiyo.
Kwa kipindi cha uongozi wao kuanzia mwaka 2020 hadi 2025, Halmashauri hiyo imefanikiwa kuongeza mapato ya ndani kutoka shilingi bilioni 1.5 hadi kufikia shilingi bilioni 5 kwa mwaka mchango ambao Menejimenti ya Halmashauri umeutambua kama wa kihistoria.
Akizungumza kwa niaba ya Madiwani wenzake, Mhe. Oitesoi alisema kuwa mafanikio hayo yamechangiwa na ushirikiano wa karibu baina ya Baraza la Madiwani na Menejimenti ya Halmashauri. Alisisitiza kuwa wamefanya kazi kwa mshikamano na kuweka mbele maslahi ya wananchi wa Wilaya ya Longido.
Makamu Mwenyekiti Mhe. Peter Lekanet, kwa upande wake, alieleza kuwa uongozi wao ulilenga kuimarisha misingi ya amani, uwajibikaji na utulivu kazini ili kuwezesha watumishi kufanya kazi kwa bidii zaidi.
Nae, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri, Bw. Nassoro Shemzigwa, alitoa salamu za shukrani kwa niaba ya menejimenti, akiwahakikishia viongozi hao kuwa kazi waliyoifanya imeacha alama isiyofutika katika historia ya halmashauri hiyo.
Akizungumzia kuondoka kwao, Bw. Shemzigwa alisema kuwa hatua hiyo ni sehemu ya maandalizi ya mchakato wa uchaguzi unaotarajiwa kufanyika Oktoba 2025, na kwamba menejimenti inaichukulia kama mapumziko ya muda mfupi kwa viongozi hao.
“Kwa kweli tunaamini kwamba huu si mwisho, bali ni mapumziko ya muda. Ni matumaini yetu kama Menejimenti kwamba tutawaona tena, tukiendelea kushirikiana katika kusukuma mbele gurudumu la maendeleo ya Halmashauri yetu,” alisema kwa matumaini.
Kwa ujumla, kikao hicho kimeacha taswira chanya ya mshikamano kati ya watumishi na viongozi waliomaliza muda wao, hali inayowapa matumaini wananchi wa Wilaya ya Longido juu ya mustakabali wa maendeleo ya wilaya yao.
Arusha- Namanga Road, Longido Town
Postal Address: S.L.P 84 Longido Arusha
Telephone: 027-2539603
Mobile: 0756395889
Email: ded@longidodc.go.tz
Copyright ©2016 Longido DC . All rights reserved. Designed by Loth Zacharia & Joseph Peter Mkumbwa Sponsored by GWF TAMISEM