NA MWANDISHI WETU, LONGIDO
Serikali imeimarisha mifumo ya ukusanyaji wa mapato katika Halmashauri ya Wilaya ya Longido kwa kutumia mashine za kielektroniki (POS) na kuanzisha mfumo mpya wa TAUSI, hatua inayolenga kuongeza ufanisi, uwazi na kudhibiti upotevu wa mapato.
Hatua hiyo imetangazwa Januari 30, 2026 na Mkuu wa Wilaya ya Longido, Mhe. Salum Kalli, wakati akiwasilisha Taarifa ya Utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa kipindi cha Januari hadi Desemba 2025 katika Kikao cha Halmashauri Kuu ya CCM Wilaya kilichofanyika katika Ukumbi wa Halmashauri.
“Ndugu Mwenyekiti, ili Wilaya iweze kutoa huduma bora kwa wananchi, ni lazima ukusanyaji wa mapato uzingatiwe kwa umakini na ufanisi. Serikali imeimarisha mifumo ya ukusanyaji kwa kutumia mashine za kielektroniki sambamba na kuanza matumizi ya mfumo wa TAUSI,” alisema Mhe. Kalli.
Alisema maboresho hayo yameongeza uwazi na uwajibikaji, yameziba mianya ya upotevu wa mapato na kuwezesha upatikanaji wa taarifa sahihi za mapato na matumizi kwa wakati.
Aidha, alibainisha kuwa uimarishaji wa mifumo hiyo umeziwezesha Mamlaka za Serikali za Mitaa kuboresha utoaji wa huduma na kuongeza imani ya wananchi kwa Serikali kwa kuzingatia misingi ya utawala bora.
Akieleza mwenendo wa makusanyo ya mapato ya ndani, Mhe. Kalli alisema mwaka wa fedha 2021/2022 Halmashauri ilikusanya shilingi bilioni 2.21, mwaka 2022/2023 bilioni 2.61, na mwaka 2023/2024 bilioni 2.74.
Aliongeza kuwa mwaka wa fedha 2024/2025 makusanyo yaliongezeka hadi shilingi bilioni 5.12, wakati makisio ya mwaka 2025/2026 ni shilingi bilioni 5.22. Hadi sasa kiasi kilichokusanywa ni shilingi bilioni 2.41, sawa na asilimia 46 ya lengo.
Mhe. Kalli alieleza kuwa matarajio ni kuvuka lengo ifikapo mwisho wa mwaka wa fedha 2025/2026 na kuweka rekodi mpya ya makusanyo.
Arusha- Namanga Road, Longido Town
Postal Address: S.L.P 84 Longido Arusha
Telephone: +255 272 970 793/ 94
Mobile: 0756395889
Email: ded@longidodc.go.tz
Copyright ©2016 Longido DC . All rights reserved.